Ukimya wa Lowassa,Sumaye na Mbowe Kuhusu MAJIPU Yanayotumbuliwa na Magufuli Wazua Maswali

Ukimya wa wanasiasa walioongoza harakati za kupambana na ufisadi katika majukwaa ya kisiasa, wakati huu Serikali ikichukua hatua za wazi na haraka kukabiliana na ubadhirifu wa mali za umma, umeibua maswali kuhusu uzalendo kwa nchi yao.

Miongoni mwa wanasiasa waliohusishwa na maswali hayo ni pamoja na aliyekuwa Waziri Mkuu, Frederick Sumaye, Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema, Freeman Mbowe na mgombea urais wa Chadema, Edward Lowassa.

Akizungumzia sakata hilo jana, Mhadhiri Mwandamizi wa Masuala ya Siasa na Utawala wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Benson Bana, alisema kama kweli ni wazalendo, ni vyema wale wote waliokuwa wakipinga ufisadi wajitokeze hadharani, kupongeza hatua zinazoendelea kuchukuliwa.

Profesa Bana alisema hali inavyoendelea nchini kwa sasa ni wazi kwamba Rais John Magufuli, anapaswa kuungwa mkono na wote waliokuwa wakipinga ufisadi na ubadhirifu serikalini. 
  
Ni wakati muafaka sasa wale wote waliokuwa wanapinga ufisadi wakiwemo wanasiasa, wajitokeze hadharani kumuunga mkono Rais wetu, kama kweli walisema hayo kwa uzalendo na uungwana,” alisisitiza Profesa Bana.

Alisema ni wakati sasa wa Sumaye, Lowasa, Mbowe na wengine waliokuwa mstari wa mbele kueleza umma ufisadi na ubadhirifu serikalini kwenye kampeni za kuwania urais mwaka 2015, wakajitokeza hadharani kupongeza kazi inayofanyika.

Pia aliwataka wote waliosema hawataunga mkono serikali iliyoko madarakani, kufuta mara moja kauli yao, kwani yanayoendelea kufanywa ni mambo mazuri kwa ajili ya ustawi wa Watanzania wote bila kujali itikadi zao.

Magufuli na Ilani ya Ukawa 
“Yapo maneno kwamba Rais Magufuli anatekeleza ilani za vyama vingine na si ya CCM, haya maneno yapuuzwe ni kukosa hoja, ilani za vyama vyote vya siasa vinavyojitambua, zinajibu maswali haya ya wananchi,” alisema Profesa Bana.

Akifafanua hilo, Profesa Bana alisema kuna maneno yanaendelea kuzunguka kwa njia ya ujumbe mfupi wa simu au kwenye mitandao ya kijamii, kuwa Dk Magufuli anatekeleza ilani za vyama vingine vya siasa na kusisitiza hoja hiyo haina mashiko.

Alisema Dk Magufuli anatekeleza yale aliyoahidi kwenye kampeni alipokuwa akiwania nafasi hiyo, kwa kuwa yapo kwenye Ilani ya CCM, huku akisisitiza kuwa ilani za vyama vya siasa mwaka huu zilifanana kwa njia moja au nyingine.

“Sisi tulipata bahati ya kusoma na kuchambua ilani za vyama vitatu CCM, Chadema na ACT-Wazalendo, tulipopitia ilani za vyama hivyo na vingine vilivyoshiriki kwenye uchaguzi uliopita, tulibaini zote zinafanana,” alisema Profesa Bana.

Alisema kama kuna chama kinasema ilani inayotekelezwa ni yao, wangekuwa mstari wa kwanza kujitokeza hadharani kumuunga mkono Rais Magufuli kwa kutekeleza hayo, lakini kukaa kimya kunazua maswali mengi. 
  
Wajuta kutompa kura 
Alisema ni vyema Rais apewe nafasi aendelee kutekeleza anayofanya kwa sababu anajibu maswali ya wananchi yaliyokuwa yakisubiriwa kwa muda mrefu na kwamba wapo baadhi ya wananchi wanajuta hivi leo kwa kutompigia kura.

Tunazungumza na watu mbalimbali wanatuambia wanajuta kumnyima kura Rais Magufuli, kwa sababu kama asingeshinda, nchi ingekosa kiongozi mzuri na mwenye kasi ya maendeleo kwa wote,” alisema Dk Bana.

Wapenda utajiri 
Mhadhiri mwingine wa chuo hicho, Profesa Kitila Mkumbo alitoa mwito kwa Watanzania wote kumuunga mkono Rais Magufuli kwa kubadilisha mitazamo yao ya kupenda vya bure, bali wafanye kazi kwa bidii.
  
Profesa Mkumbo alisema juhudi zinazofanywa na Rais Magufuli, zitakuwa na tija zaidi iwapo Watanzania wote watamuunga mkono kwa kubadilisha mitazamo yao ya kupenda utajiri wa haraka haraka.

Jitihada za Rais Magufuli pekee hazitoshi, bali jamii yote ya Tanzania lazima ibadilike, tuache kufanya vitu kwa mazoea na kupenda vya bure na utajiri wa haraka haraka, bali tupende kufanya kazi kwa bidii,” alisema Profesa Mkumbo.

Alisema masuala ya ubadhirifu na ufisadi ni mambo sugu yanayosumbua nchi na hatua zilizoanzwa kuchukuliwa na Rais Magufuli ni nzuri kwani tofauti na serikali zilizopita, yeye anatekeleza kwa kasi zaidi.

Ubadhirifu ni tatizo sugu nchini, lilianza kufanyiwa kazi tangu enzi za Mwalimu Nyerere hadi Rais mstaafu Jakaya Kikwete, ila kwa awamu hii ya Rais Magufuli, yeye anatekeleza kwa kasi zaidi,” alisema Profesa Mkumbo.
Previous
Next Post »